ENDELEENI KUWATETEA AMBAO WAMEIACHA YANGA IKIENDA ALGERIA LAKINI HAWATA UKWEPA USALITI




NA SALEH ALLY
YANGA imefunga safari kwenda nchini Algeria kuwavaa USM Alger ya nchini humo katika moja ya mechi ngumu kabisa za Kombe la Shirikisho.

Kikosi cha Yanga kimeondoka kinatia huruma, kikiwa na upungufu wa wachezaji kwa kuwa wachezaji wake baadhi wameamua kutokwenda kutokana na masuala kadhaa.

Wachezaji hao wameona wasiende Algeria kwa kuwa kila mmoja ana madai yake lakini suala lao limefanywa la kificho kwa kiasi fulani.

Ingawa mambo yanakwenda kwa uficho lakini tunajua, Yanga ni klabu ya watu na wenyewe ni Watanzania, hivyo hata kama jambo litafichwa vipi, mwisho itajulikana tu.

Juhudi za viongozi zimeonekana wanataka kutuliza mambo yaende kwa mwendo wa kawaida kidogo, tumewaona wanajaribu kuwatetea wachezaji ili waonekane hawajafanya jambo baya.

Inawezekana wanaumia, lakini nao wanaona aibu kwa kushindwa kuwa watekelezaji wazuri wanaoweza kufanya mambo vizuri na mwisho kuepusha hizo kero kama ambazo zinazojitokeza.

Hivyo, ili kuficha mambo na kutengeneza utulivu, basi ni juhudi za kuficha mambo ili iwe salama kwa wote. Si jambo baya kwa kiongozi kutengeneza busara na kufanya mambo kwenda kwa mwendo mzuri.

Pia si vizuri kuficha ukweli kwa kuamini unayafanya mambo vizuri wakati unaharibu kwa faida ya wachache huku ukijua si kutenda haki.

Taarifa zilizopo, wachezaji hasa wale nyota au tegemeo waliogoma kuondoka ni kwa sababu ya mishahara yao ya miezi kadhaa. Tumeelezwa ni miezi mitatu, lakini hata kama itakuwa ni miezi miwili au mmoja, bado ni mishahara na wanadai.

Kama hawajalipwa kweli, basi wana haki, wanastahili kulipwa na kama hawajalipwa basi hii si sahihi, walipwe. Maana wanafanya kazi yao wanapambana na wanaumia, hivyo haki yao si jambo la kubembeleza.

Pamoja na hivyo, bado ninarudi katika msimamo wangu uleule kwa kuwa katika hili si jambo geni ninaloliandika kwamba kama umecheleweshewa mshahara, hauwezi kususa kazi na kuacha chombo unachokiendesha, kiende mlama.

Binafsi naona kufanya hivyo ni usaliti, naita usaliti kwa kuwa unakubali unachokitumikia kitumbukie shimoni, hii ni kuonyesha hauna mapenzi ya dhati na hasa kama unagoma katika kipindi cha uhitaji mkubwa.

Yanga uliyoipigania iingie hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho. Leo unagoma kwenda kuitumikia hata kama itafeli. Je, kama utalipwa mishahara yako hapo baadaye, hii ya siku ambazo uliisaliti Yanga halafu ikaenda, mfano ikafungwa, utailipa nini? Utachukua mshahara wa siku hizo?

Nakubaliana na watu kudai haki zao, lakini bado kuna njia sahihi, angalau wachezaji wangeenda kuipigania Yanga halafu wangerudi baada ya mapambano na kuitisha mkutano wa waandishi wa habari na kuomba wasaidiwe na Wanayanga na Watanzania kutokana na hali waliyonayo, mimi ningewaelewa.

Kuacha Yanga izame, maana yake bado huna mapenzi. Hivyo kuna kila sababu ya Yanga kuangalia upya tena watu walionao kama kweli wapo kwa nia ya klabu. Kwa viongozi pia, basi waonyeshe hawajafeli kwa kuwa waendako, chombo kitaenda mlama zaidi ya hapa na mwisho kuzama.

YONDANI:
Huyu mkataba wake umeisha kwa zaidi ya mwezi na sasa, ajabu uongozi umeshindwa hata kukaa naye mezani pamoja na umahiri wake. Ameamua kukaa kando licha ya kuelezwa kwamba anaumwa.

TSHISHIMBI:
Kuna taarifa za ndani zinaeleza kweli Mkongo huyu ameumia na hata mechi dhidi ya Simba alicheza akiwa mgonjwa. Bado suala la mshahara limechangia aumwe zaidi.

AJIBU:
Imeelezwa hakuwa na ugonjwa wa kushindwa kwenda, kama ni maumivu aliyonayo na mshahara wake ungekuwa umetoka, basi angejitutumua na kuungana na wenzake Algeria.

CHIRWA:
Inajulikana huyu si mara ya kwanza, aliwahi kususa na kwenda kwao Zambia, viongozi wakamtetea lakini ikajulikana. Amerudia na huenda anaona ni jambo rahisi na haoni shida, aliishaitoa Yanga Kombe la Mapinduzi na mshahara wake akalipwa.

CANNAVARO:
Hongera kwa kujitolea Yanga, lakini inaelezwa ana matatizo ya kifamilia. Kweli sasa, kipindi ambacho Yanga inakwenda kuivaa timu ya Algeria, vipi nahodha? 

KAMUSOKO:
Tunaambiwa ni majeruhi, lakini tunajua alishaanza kucheza na hakukuwa na taarifa ya kuumia kwake. Hakuna ubishi, suala la utata wa mishahara, naye yumo lakini kumbuka amekuwa nje zaidi ya hiyo miezi mitatu anayodai, na amevumiliwa!

ENDELEENI KUWATETEA AMBAO WAMEIACHA YANGA IKIENDA ALGERIA LAKINI HAWATA UKWEPA USALITI ENDELEENI KUWATETEA AMBAO WAMEIACHA YANGA IKIENDA ALGERIA LAKINI HAWATA UKWEPA USALITI Reviewed by Unknown on 3:44 PM Rating: 5

No comments:

Theme images by Colonel. Powered by Blogger.