Adios Twite, vazi la ukimataifa limekutoa Jangwani

img_0095
Na Abdul Mkeyenge
NIMEREJEA zangu Dar es Salaam jana jioni na leo asubuhi nimeamka mapema nikiwa na kazi moja tu. Nina kazi ya kuitafuta shajara yangu inayomuhusu Mbuyu Twite, kile kipande cha baba cha Yanga chenye damu ya Kongo na kiliwahi kuvaa jezi za timu ya taifa Rwanda ‘ Amavubi ‘.
Katika pitia pitia shajara mbele ya meza iliyofutwa vyema pembeni kukiwa na kikombe cha kahawa na vitabu vya Ben Mtobwa naenda kurasa niliyoandika neno historia na moja kwa moja nakutana na kitu kinachoitwa usajili wa Twite. Haraka sana nafungua kurasa hiyo na nakukumbuka Agosti 30 siku ya Alhamisi mwaka 2012, Twite ndio alitua uwanja wa Ndege wa Mw. Nyerere na kulakiwa na manazi wa Yanga waliomvesha jezi namba 4, huku jezi hiyo ikiandikwa jina la aliyekuwa Mwenyekiti wa Simba Ismail Aden Rage, wakati huo.
Nderemo, vifijo, raha na mikogo vilitamalaki uwanjani hapo na Twite mwenyewe hakuwa na mengi ya kusema zaidi ya kushukuru kila mmoja aliyeenda kumpokea na kusema ” Kujia kwa watu wingi kwa ajili ya kunipokea inaonyesha Yanga ni timu kubwa na hii itanifanga kufanga kazi nzuri kwa bidii. Naomba ushirikiano huu udumu na kung’a kitu tutafanga kama timu” alisema Twite ambaye alizungumza kwa kiswahili kigumu kidogo.
Maneno haya yalitoa milipuko ya kelele kwa watu wa Yanga waliokuwa uwanjani pale wakimsikiliza na yalikuwa shubili upande wa Simba ambao nao walitajwa kumsajili na walishaitengeneza hadi jezi yake na kuiuza katika tamasha lao la kila mwaka la Simba Day.
Mashabiki wa Simba wakati huo waliamini kumpata Twite kutaenda kuwapoza machungu ya kumpoteza mlinzi wao kinga’ng’anizi Kelvin Yondani ambaye alitimkia Yanga.
Usajili wa Twite Yanga uliwatoa povu watu wa Simba. Mara nyingi kwenye majukwaa yao Twite alikuwa na maisha magumu. Alizomewa na kila mmoja na mwishowe akawa anaitwa jina la Mwizi. Jina hili lilidumu na lilikuja kupungua makali Simba ilipomsajili Juuko Mursheed.
Lakini Simba ilipokuwa na mabeki Komambil Keita ( Mali ), Lino Musombo ( Congo ), Obadia Mungusa ( Tanzania ) Pascal Ochieng ( Kenya), jina la Mwizi halikukauka vinywani mwa mashabiki wa Simba.
Kufumba na kufumbua yule Twite aliyewadengulia Simba na kuwapa pepo ndogo Yanga ametemwa Yanga na nafasi yake imechukuliwa na Justice Zullu waliomuona wanamuita Mkata Umeme.
Maisha ya mpira ndio yako hivi. Kuna wakati yanakuwa hivi na wakati yanakuwa vile. Kalamu yangu haiamini kilichofanya Twite anyimwe mkataba mpya ni uwezo wake kushuka au kama wasemavyo wengine umri mkubwa.
Twite bado ana nishati ya kucheza Ligi yetu kwa misimu mitatu mbele bila matatizo. Tukiri leo. Ligi yetu ni dhaifu na haiwezi kumshinda mchezaji anayejitambua kama Twite kucheza vyema na kuisaidia timu kupata mataji. Kama tunakiri Twite hana nishati ya kucheza ligi yetu hapo hapo tujiuluze ni mchezaji yupi wa Tanzania anayemkaribia kwa ufiti?
Wachezaji wa aina yake hawako tena siku hizi. Tuna wachezaji wepesi ambao hawako fiti. Kando ya Twite unaweza kumpata kiraka wa Azam yule mwenye moyo wa Simba na miguu ya chuma Himid Mao. Angalau Himid anaweza kupishana na Twite linapokuja suala la ufiti.
Kilichomuondoa Twite ni idadi 7 ya wachezaji wa kigeni. Hapa kulikuwa hakuna namna ilikuwa lazima aache nafasi yake iende kwa Zullu nae aondoke. Unadhani Twite angezaliwa kwetu Rufiji angeondoka Yanga na kumuacha Said Makapu? Kuzaliwa Kinshasa ndio kumemnyima mkataba.
Timu nyingi zinatamani huduma yake. Amini hili. Hata hao waliokuwa wakimzomea hawakumzomea kwa kuwa Twite alikuwa hajui mpira,  walimzomea ni kutokana na kuwahi kuwauzi.
Licha ya hivyo malipo ya Dola Elfu mbili kwa TFF nayo ni sababu nyingine inayofanya baadhi ya timu kuishia kumtamani kutokana na kutokuwa na uwezo wa kumlipia fedha hizo.
Twite anakupa vitu vingi mchezoni. Anakupa faida ya kujilinda na kushambulia, huku akiwa na faida ya ziada ya kucheza namba nyingi kwa wakati mmoja. Unadhani angekuwa Mndengereko kama mimi Yanga ingemuacha? Isingemyacha.
Faida yake nyingine ni mipira ya kurusha. Yanga imevuna mabao mengi kwa mtindo wake wa kurudi nyuma na kurusha mipira ambayo mingi inakuwa madhara langoni mwa wapinzani. Yanga walikuwa na style nyingi za kupata mabao. Kuondoka kwa Twite wamepunguza style moja.
Mipira ya kurusha ina faida. Ukitaka kuliamini hili tembelea uwanja vya Britania Stadium pale England kisha taja jina la Delap. Delap aliishi katika sayari yake lilipokuja suala la kurusha mipira na kuipa timu ushindi.
Lakini nyumbani Twite alibezwa na baadhi ya mashabiki na akaitwa jina la mcheza rede kutokana na style hiyo. Ninachoamini kilichomtoa Twite ni ‘uwepesi’ wake katika wachezaji wa kigeni wa Yanga walioko sasa.
Unaanzaje kufikiria kulikata jina la Niyonzima ambaye anatajwa kama Nyerere wa Jangwani? Inasemekana Niyonzima ndio aliyesababisha mmoja ya kiongozi kujiuzulu nafasi yake, mchezaji huyu unaanzaje kumgusa wewe Lwandamina au Hans?
Tuwakate Donald Dombo Ngoma na Thaban Skalah Kamusoko na kumpisha Zullu? Hapana! Tuwakate Tambwe Amissi Jocelyn na Vicent Bossou kumpisha Zullu? Hapa hakukuwa na namna nyingine ilikuwa ni lazima Twite awe mbuzi wa kafara ili maisha mengine yaendelee Jangwani.
Nilitamani kuendelea kumtazama Twite akiwa na Yanga, lakini kwa hali iliyoko sioni wapi naweza kumuona kwa wakati huu zaidi ya kwenda kesho uwanja wa Uhuru kumtazama katika mchezo maalum dhidi ya JKU ambao utakuwa wa kumuaga.
Nitaenda kuutazama mchezo huu kwa sababu mbili. Mosi kuagana na Twite ambaye namtakia maisha mema huko aendako na pili kumtazama huyo Zullu ‘Mkata Umeme’.
Rafiki yangu  Peter Kadutu siku za karibuni amekuwa akijifunza Kihispanyola na moja ya maneno niliyowahi kuyapata kwake ni neno la Adios likimaanisha kwaheri. Si vibaya nami nikimuaga Twite kwa kumwambia Adios Twite, vazi la ukimataifa limekutoa Jangwani.
Adios Twite, vazi la ukimataifa limekutoa Jangwani Adios Twite, vazi la ukimataifa limekutoa Jangwani Reviewed by Unknown on 6:18 AM Rating: 5

No comments:

Theme images by Colonel. Powered by Blogger.